Daraja
la Mtambaswala linaloziunganisha nchi ya Tanzania na Msumbiji, linavyoonekana.
Daraja la Mtambaswala linaloziunganisha nchi ya Tanzania na Msumbiji.
Wananchi wakiwa chini ya Daraja
la Mtambaswala linaloziunganisha nchi za Tanzania na Msumbiji. (Picha zote na Aron Msigwa-Maelezo)
Na
Benedict Liwenga, MAELEZO-DSM.
17/09/2014.
KAMA utakuwa umeshawahi kuishi ama kutembelea
mkoa wa Mtwara kipindi cha miaka ya Sabini mpaka mwishoni wa miaka ya tisini na
kufanikiwa kuuona ama kuwepo katika mkoa huo kwa kipindi cha karibuni,utakuwa
sambamba nami kifikra juu ya usemi unaolindima kwa sasa ndani ya mkoa huo usemao
“Mtwara kuchele”, yaani kwa maelezo mengine maana yake “Mtwara kumekucha”.
Kwa
mujibu wa Ramani ya Tanzania, mkoa huo wenye watu wakarimu, wenye kuuenzi
utamaduni wao na asili yao, uko katika pembe ya Kusini-Mashariki kabisa ya nchi.
Umepakana na Mkoa wa Lindi kwa upande wa
kaskazini, Bahari
ya Hindi kwa upande wa Mashariki, nchi ya Msumbiji kwa upande wa
kusini na Mkoa
wa Ruvuma kwa upande wa Magharibi.
Mtwara ni miongoni mwa mikoa midogo nchini Tanzania ukiwa
na kilometa za mraba 16,720 na una jumla ya wakazi 1,128,523 kwa mujibu wa sensa
ya 2002.
Kati ya makabila yanayopatikana ndani ya mkoa wa Mtwara Wamakonde wanajulikana zaidi kutokana na sanaa
yao ya uchongaji vinyago,
pia yapo makabila ya Wamakuwa na Wayao.
Wilaya zipatikanazo katika mkoa huo ni Wilaya ya Mtwara Mjini, Mtwara
Vijijini, Masasi, Nanyumbu, Newala na Tandahimba ambapo ndani yake ndipo tarafa 21,
kata 98 na Vijiji 554 huzaliwa.
Mtwara ilikuwa kati ya mikoa iliyobaki nyuma kimaendelea kwa miaka mingi kutokana
na ugumu wa mawasiliano ya barabara isiyopitika kwa sehemu kubwa ila baada ya
kujengwa kwa Daraja la mto Rufiji lijulikanalo kama Daraja la Mkapa mnamo mwaka
2002 pamoja na ukarabati unaoendelea kwa barabara zote zinazounganisha
mkoa huo pamoja na kujengwa na daraja linalounganisha mkoa wa Mtwara na nchi ya
Msumbiji lijulikanalo kama daraja la Mtambaswala na kupelekea kukua kwa uchumi
wa mkoa huo.
Kwa sasa upatikanaji wa bidhaa mbalimbali kiurahisi kutoka mikoa tofauti unafanyika
kirahisi na kupelekea kukuwa kwa shughuli za kibiashara ndani ya mkoa huo.
Mtu akitaka kwenda Mtwara toka Dar es salaam kwa barabara atachukua masaa
manane tu, tofauti na miaka ya Sabini mpaka miaka ya tisini ambapo ilikuwa
inakuchukuwa zaidi ya siku mbili mpaka tatu kwa barabara, pia usafiri wa wa
ndege unapatikana kwa wepesi zaidi katika mkoa huo wa Mtwara ambapo walau kila
kukicha ndege za abiria zimekuwa zikifika mkoani hapo.
Hatuwezi kuuzungumza Mkoa wa Mtwara kinagaubaga tukaiweka kando historia ya
Mkoa huu juu ya kumbukumbu ya jaribio la
Waingereza la kuanzisha mradi mkubwa wa maendeleo katika eneo hilo
ambalo lilishindikana kwa kipindi hicho cha mkoloni.
Taarifa zinasema kuwa kuanzia 1947 Serikali ya kikoloni ilijenga Bandari ya
Mtwara pamoja na reli lakini vile vile waliweza kuupanga mji wa Mtwara Mikindani vizuri na serikali ya mkoloni ikaamua
kuanzisha kilimo cha mashamba makubwa kwa ajili ya karanga hasa zilizohitajika
kwa ajili ya mahitaji ya Waingereza ya mafuta ya kupikia.
Mradi huu ulikuja kushindikana kabisa na pesa nyingi zilipotea kiasi mradi huo
kufutwa kabla ya Tanzania kupata Uhuru wake, pia reli ya Kusini ilikuja
kuondolewa mnamo mwaka 1963.
Ni dhahiri kuwa
kwa sasa Mtwara kumekucha na mwangaza wa matumaini ya ushindi dhidi ya
umasikini uliotamalaki kuwa ni ndoto baada ya nyota kuu tatu zinazoweza kuondoa
giza la kiuchumi mkoani Mtwara kung’ara, ambazo ni Bandari, zikiwemo shughuli
za sekta za Mafuta na Gesi.
Ndani ya mkoa huo,
hizo ni nyota za mapambazuko ya kiuchumi kwani hatua nyingine kubwa zimepigwa
mkoani humo baada ya hivi karibuni Bandari yake kuingia katika mchakato wa kuwa
Eneo huru la biashara.
Waziri wa Uchukuzi,
Dkt. Harrison Mwakyembe alisema kuwa, kufanywa kwa Mtwara kuwa na eneo la
Bandari Huru ni fursa kwa Makampuni kote duniani kuwekeza mkoani humo ili
kuhudumia Mashirika yanayohusika na shughuli za gesi asilia na mafuta.
“Nawasihi wote
wanaohusika wafanye maandalizi yanayohitajika ili wenye kutaka kuja kuwekeza
waweze kufanya hivyo bila vikwazo,” alisema Dkt. Mwakyembe.
Dkt. Mwakyembe,
aliongeza kuwa Bandari hiyo itawezesha kufanyika kwa biashara ya maeneo ya
mbali ya Kusini na Mashariki mwa Afrika, yakiitumia Bandari hiyo kama kitovu
cha biashara.
Chini ya Mkataba
kati ya Mamlaka za Bandari Tanzania (TPA) na Export Processing Zone Authority (EPZA),
jumla ya eneo lenye ukubwa wa hekta 110 limetengwa kwa ajili ya uwekezaji
katika shughuli za gesi na mafuta huku zikivuta kampuni za Kimataifa mbalimbali
zikiwemo; Schlumberger, Weatherford, Halliburton International Inc za nchini
Marekani, pia kampuni ya Lena, FFF (T), Alpha Group, Tans Ocean Industries
& Services, Queensway kutoka Dubai na Uingereza; Altus Tanzania Ltd kutoka
Singapore na Inter-shore Tanzania Ltd ya Afrika Kusini bila kukisahau Kiwanda
cha Cement cha Dangote.
Kampuni hizo
zinaongeza idadi katika kampuni nyingine kubwa ambazo zimekuwa zikiendesha
shughuli zake za awali mkoani Mtwara kama BG Group, Exxon Mobil, Statoil,
Petrobras, na nyingine kama Ophir Energy, Ndovu Resources, na Maurel &
Prom.
Nyaraka kadhaa
zilizoandaliwa mwaka 2012 na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, zinaonyesha kuwa,
katika kipindi cha miaka mitano hadi minane ijayo mkoa huo utakuwa Kitovu cha Uchumi
unaoendeshwa kwa Gesi Asilia na mazao yatokanayo na gesi na mafuta kwa eneo
lote la Afrika Kusini Mashariki kwa maana ya Congo DRC, Malawi, Msumbiji,
Tanzania na Zambia.
“Bandari ya
Mtwara ni lango la asili kwa biashara za Kimataifa yenye uwezo wa kuhudumia
eneo tajiri kwa maliasili la Kusini Mashariki mwa Afrika lijulikanalo kama
Ukanda wa Maendeleo wa Mtwara (Mtwara
Development Corridor) uliosambaa katika maeneo ya kijiografia ya Malawi ya
Kati na Kaskazini, Kaskazini mwa Msumbiji, Kusini mwa Tanzania, Kaskazini mwa
Zambia na Kusini Mashariki mwa Congo DRC,” Alisema Dkt. Mwakyembe.
Nyaraka zinaeleza
pia, ukiacha kwamba Mtwara itakuwa kitovu cha shughuli za utafutaji na uzalishaji
gesi asilia na mafuta.
Chini ya mpango
wa muda mrefu wa Mtwara Development Corridor, mkoa huo utahusika na usafirishaji
na uwekezaji wa miradi mikubwa ya madini kama vile Nickel, Uranium, Chuma,
Titanium, Shaba pamoja na Makaa ya mawe yanayokadiriwa kuwa yataongeza tani za
mzigo zipatazo milioni 15 kila mwaka zote zikipita katika Bandari ya Mtwara.
Tayari Kampuni
ya Sichuan Hongda Group kutoka China na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC)
wameingia mkataba wa dola za Marekani bilioni tatu katika mradi wa ubia wa
kuendeleza hazina ya madini katika eneo la Liganga na makaa ya mawe katika
maeneo ya Mchuchuma na Ngaka.
Pia tayari kazi
imeanza ya ujenzi wa kiwanda cha Saruji cha Dangote kitakachozalisha meta
milioni tatu pembezoni mwa mji wa Mtwara.
Taarifa
zinaendelea kueleza kuwa Kiwanda hicho kinatarajiwa kuzalisha hadi tani milioni
saba ifikapo mwaka 2018, na hiyo ni sehemu ya taarifa shughuli
zilizokwishakuanza na ambazo zitaendelea kwa miaka mingi ijayo mkoani humo na
maeneo yake ya jirani.
Kutokana
kukucha kwa mkoa wa mtwara kunakotokana na kuchanua kwa mazingira ya kiuchumi
kwa uwepo wa bandari ya asili na yenye kina kirefu Afrika Mashariki pamoja na
ugunduzi wa mafuta na gesi alikadharika na kuunganisha mkoa wa Mtwara na mikoa
mingine chini ya mradi wa Mtwara Development Corridor wawekezaji mbali mbali
wakubwa na wadogo wanajisogeza ndani ya mkoa huo kuwekeza na kuufanya ukuwe
kiuchumi zaidi.
Hivi
sasa kuna
ujenzi wa nyumba za makazi na majengo ya biashara kwa wingi kutokana na
ongezeko kubwa la wageni wanaokuja kufanya biashara na wengine kuajiriwa katika
miradi na sekta mbalimbali zinazoendelea ndani ya mkoa huo.
Tayari benki mbalimbali kama vile CRDB
Bank imaahidi kufungua tawi katika eneo la Kiwanda cha Dangote ambapo
itawezesha wafanyakazi wa eneo hilo kupata huduma za kibenki kwa urahisi lakini
pia Benki Kuu ya Tanzania (BOT) wanajenga ghorofa kwa ajili ya ofisi zao.
Ujenzi wa hoteli za kisasa umeshamiri kwa ajili ya kuhakikisha kuwa
wageni wanaofika mkoani humo kila kukicha wanapata mahala pazuri pakupumzika kitu
ambacho hupelekea biashara ya hoteli kukua pamoja na nyumba na hasa thamani ya
ardhi kupanda mara dufu.
Ndani ya Manispaa ya Mtwara Mikindani miundombinu ya barabara za lami imeongezeka kutoka nne zilizokuwepo mwaka juzi na ambapo kwa sasa Benki ya Dunia imefadhili ujenzi wa barabara kadhaa ambazo pia zitawekwa taa za barabarani kama ilivyo katika Majiji mengine hapa nchini.
Ndani ya Manispaa ya Mtwara Mikindani miundombinu ya barabara za lami imeongezeka kutoka nne zilizokuwepo mwaka juzi na ambapo kwa sasa Benki ya Dunia imefadhili ujenzi wa barabara kadhaa ambazo pia zitawekwa taa za barabarani kama ilivyo katika Majiji mengine hapa nchini.
Nikiwa shuhuda wa haya, nimeweza kuona Ujenzi
wa barabara ziendazo Soko la Samaki (Ferry) kijulikanacho kama Kivuko cha
kwenda Msanga Mkuu, pia nimeambiwa kuwa uundwaji wa kivuko hicho unaendelea
vizuri.
Aidha, Kivuko cha Kilambo kwenye Mto
Ruvuma kuelekea nchi ya Msumbiji kimekwishamilika.
Sambamba na hayo, Serikali imekwishaweka
mpango wa upanuzi wa Uwanja wa Ndege mkoani humo ili usafiri uzidi kuwa wa
urahisi kwa ndegelakini pia ukpo usafiri mzuri wa mabasi ya kisasa yatokayo
Mtwara kwenda Dar es Salaam pamoja na wilaya zilizopo jirani na mkoa lakini jambo
lililo zuri zaidi, katika mkoa huo ni kwamba hakuna mgao wa umeme.
Hali ya uwepo wa Vituo vya redio ni ya
kuridhisha kwani kwa sasa vituo vingi vya redio vimefunguliwa na vinaendelea
kufanya kazi ya kuhabarisha Umma.
“Ama kweli Mtwara kuchele!!!”
“Ama kweli Mtwara kuchele!!!”
No comments:
Post a Comment