TANGAZO


Monday, August 19, 2013

MANISPAA YA TEMEKE: UKUSANYAJI WA MAPATO




Ofisa Uhusiano wa Manispaa ya Temeke, Joyce Msumba, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, wakati alipokuwa akielezea utendaji kazi wa manispaa hiyo. Kulia ni Mhasibu, Kitengo cha Mapato, Zacharia Mbedule na Katikati ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari,  Zamaradi Kawawa.
Mchumi wa Manispaa ya Temeke, Edward Simon, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari kuhusu suala la ukusanyaji mapato.


Mhasibu Kitengo cha Mapato, Zacharia Mbedule, akifafanua jambo kwa waandishi wakati wa mkutano huo wa kuelezea kuhusu ukusanyaji mapato kwa manispaa hiyo.

Utangulizi
Manispaa ya Temeke ni moja kati ya Halmashauri zinazounda Jiji la Dar-es-Salaam, nyingine ni Ilala na Kinondoni, ina eneo la kilometa za mraba 656 na ukanda wa pwani wa kilometa 70. Inapakana na bahari ya Hindi kwa upande wa Mashariki, kusini na Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani, Wilaya ya Ilala kwa upande wa kaskazini na  magharibi. Ki-utawala manispaa ya Temeke imegawanywa katika majimbo mawili yaTemeke na Kigamboni , tarafa 3 , kata 30 na Mitaa 180.

Kulingana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, Manispaa ya Temeke ina jumla ya watu 1,368,881, wanaume 669,056 na wanawake 699,825. Wakazi hawa wanajishughulisha na ajira rasmi viwandani na maofisi , kilimo na sekta isiyo rasmi.

Lengo la Manispaa ya Temeke kuitisha mkutano huu,  ni ili iweze  kushirikiana na wanahabari kuuhabarisha  umma, na hasa wakazi wa Temeke juu ya ukusanyaji wa mapato na mafanikio tuliyofikia pia changamoto zinazotukabili katika kutoa huduma kwa jamii.

Ukusanyaji Mapato

Halmashauri ya Manispaa ya Temeke inategemea mapato yake kutokana na vyanzo mbalimbali, ikiwemo vyanzo vya ndani, ruzuku kutoka serikali kuu, michango ya  wadau mbalimbali  wa maendelo na wahisani , pamoja na nguvu za wananchi, ikiwa ni kwa  mujibu wa sheria ya fedha ya serikali za mitaa (Local Government Finance Act Na. 8 ya mwaka 1982).

Mapato  yake yamekuwa yakiongezeka mwaka hadi mwaka ambapo katika mwaka wa fedha 2011/2012  kumekuwa na ongezeko kubwa zaidi.
Sababu za ongezeko  na mafanikio

Ongezeko  la mapato limetokana baada ya  kuanzishwa utaratibu wa kuwa na mameneja wa vyanzo vyote vikubwa na wao kusimamia kwa karibu zaidi. Makusanyo ya mapato ya ndani yameongezeka kutoka shilingi bilioni tatu milioni mia nane tisini na moja na ishirini na tano elfu mia tatu arobaini na sita (3,891,025,346.00) mwaka 2005/2006 hadi shilingi bilioni ishirini na  tano, milioni  mia moja sabini na tano, hamsini na tatu elfu na tisa  (25,175,053,009.00) mwaka 2012/2013, ukusanyaji umefikia asilimia 112.2%  ya mapato.

Kutoa elimu kwa walipa kodi, ada na ushuru mbalimbali, na matumizi ya GIS (Geographical Information System) na MRECOM (Municipal Revenue collection Manager), kwa ajili ya kukusanya na kutunza takwimu za wanaolipa ushuru wa mabango (bill Boards), huduma za jiji ( Service levy), kodi ya Majengo  (Property tax), na nyumba za kulala wageni ( hotel levy) .

Pia kuwatambua walipa kodi wa vyanzo mbalimbali ambao wanalipa kodi ama ushuru bila shuruti, kukaa nao pamoja kujadiliana juu ya kuboresha ukusanyaji huo na kuwazawadia wanaofanya vizuri katika kulipa kodi kwa hiyari; zoezi hilo linafanyika kila mwaka kuanzia mwaka 2011/2012 ambapo kuna siku rasmi ya mlipa kodi kila mwaka ambayo ni tarehe 10 Novemba.

Toka kipindi cha mwaka 2005 hadi 2012/2013 uboreshaji wa utoaji huduma muhimu umeongezeka kama miundombinu (barabara za lami  kutoka km 166-173km), ujenzi wa masoko (3-15), shule za sekondari (5-39) na utoaji huduma za afya (zahanati  19-28), ujenzi huu umetokana na vyanzo vya ndani.

Kuhusu uzoaji taka, mwaka 2005 kiasi cha taka kilicho zolewa na kupelekwa  dampo ni tani 102,220 sawa na asilimia 39.5 ya taka zilizozalishwa (tani 258,785). Mwaka 2012 kiasi cha taka zilizozolewa na kupelekwa dampo ni tani 195,224 ambayo ni asilimia 47 ya tani 415,370 zilizozalishwa.

Changamoto

Kwa kuwa majukumu ya Serikali za Mitaa ni kutoa huduma kwa  wananchi,na kwa kuwa huduma hizo zinahitaji rasilimali fedha,bado kuna changamoto kwa Wadau wa maendeleo kushiriki kikamilifu kuunga mkono juhudi za Halmashauri yetu za kuwahudumia wakazi wake katika kulipa kodi, ushuru na ada mbalimbali zilizowekwa kwa mujibu wa sheria ili halmashauri iweze kutoa huduma bora kwa wakazi wake kwaajili ya ustawi wa maendeleo yao.

Ongezeko la idadi ya watu; hasa wahamiaji kutoka katikati ya jiji na  kutoka mikoa mingine kuhamia  Manispaa ya Temeke  katika mitaa ya  Mbagala rangi tatu , Charambe, Kongowe,Tandika, Makangarawe na maeneo mengine , hii huiongezea halmashauri mzigo wa utoaji huduma.

Ongezeko la uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na utupaji ovyo takataka.

Kuchelewa kwa ruzuku kutoka Serikali kuu, na wahisani kunasababisha mapungufu katika ukamilishaji wa baadhi ya miradi iliyopangwa kwa kipindi husika.

Ujenzi holela wa makazi, kutokana na idadi kubwa ya wahamiaji ambao wanataka kuishi maeneo ya mjini, uchache wa watendaji na vitendea kazi.

Ukusanyaji usiokidhi/kufikia malengo ya kodi ya majengo inayokusanywa na mamlaka ya mapato Tanzania (TRA)

Mikakati tuliyojiwekea

Kuhimiza wananchi na wadau wengine kuendelea kuchangia miradi inayotekelezwa katika ngazi ya jamii,hususani ujenzi wa sekondari,zahanati,barabara,visima vya maji nk.

Halmashauri itahakikisha ifikapo mwaka 2015 vyanzo vyote vya mapato vinakusanywa kupitia mifumo ya kompyuta.

Ufuatiliaji wa karibu sana utaendelea kufanyika kwa vyanzo vyote vya mapato ikiwemo Huduma za Jiji (service levy) leseni za biashara, Kodi ya Majengo (Property tax),kodi ya mabango( Bill boards), na ushuru wa nyumba za kulala wageni na  nyinginezo kwani vyanzo hivi vimeonyesha mafanikio makubwa sana kama vitafuatiliwa kwa karibu.

Halmashauri itaendelea na ushirikino wa karibu na TRA ili  kuongeza makusanyo ya mapato ya kodi ya majengo.

Na mwisho ni kuendelea kutoa elimu kwa walipa kodi kwa njia mbalimbali ili waweze kutimiza wajibu wao bila shuruti na Halmashauri iweze kutoa huduma bora.

No comments:

Post a Comment