TANGAZO


Thursday, July 4, 2013

MAMLAKA YA CHAKULA NA DAWA:TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari-Maelezo Zamaradi Kawawa(aliyesimama) akimtambulisha Msemaji wa Mamlaka ya Chakula na Dawa, Gaudensia Simwanza(katikati) wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari- Maelezo kushoto ni Salum Kindoli Mtaalam wa Maabara.
Msemaji wa Mamlaka ya Chakula na Dawa, Gaudensia Simwanza (katikati)  akieleza jambo kwa waandishi wa habari katika mkutano uliofanyika  ukumbi wa Idara ya Habari-Maelezo, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari-Maelezo Zamaradi Kawawa kushoto ni Salum Kindoli Mtaalam wa Maabara.
Picha zote na Hassan Silayo-MAELEZO)

MAELEZO KUHUSU MAFANIKIO YA  MAABARA YA CHAKULA NA MIKROBIOLOJIA BAADA YA KUPATA ITHIBATI KWA KIWANGO CHA KIMATAIFA CHA ISO/IEC 17025:2005

*      Wakurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo,
*      Waandishi wa Habari,
*      Mabibi na Mabwana.
Ndugu wanahabari,
Napenda kwa heshima na taadhima kutumia fursa hii kwa niaba ya Menejimenti ya TFDA na wafanyakazi wote kwa ujumla kuwakaribisha katika mkutano huu.  TFDA ni taasisi ya Serikali iliyopo chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii iliyoundwa chini ya sheria namba 1 ya Chakula, Dawa na Vipodozi  Sura 219 kwa lengo la kudhibiti ubora na usalama wa chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba ili kulinda afya za wananchi.
Ndugu wanahabari,
TFDA ilianza kazi rasmi tarehe 1 Julai, 2003 na kama taasisi nyingine ina dhima, dira na falsafa zake kama ifuatavyo:-
Ni ukweli usiopingika kwamba vyakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba ni bidhaa nyeti na kila mmoja wetu ikiwa ni pamoja na familia zetu tunazitumia kila siku. Hata hivyo, kama hazikudhibitiwa ipasavyo matumizi ya bidhaa hizi yanaweza kuleta madhara makubwa ikiwa ni pamoja na kusababisha ulemavu, kupoteza maisha na hata kudhoofisha uchumi wa nchi.
TFDA kama taasisi iliyopewa dhamana ya usimamizi wa bidhaa hizo inahakikisha kwamba vyakula, dawa (ikiwa ni pamoja na dawa za mitishamba), vipodozi na vifaa tiba vinavyouzwa katika soko la Tanzania vinakidhi viwango vya usalama, ubora na ufanisi.
Hivi sasa TFDA inatambuliwa kwa kufanya kazi kulingana na viwango vya kimataifa vya ISO 9001: 2008.
Ndugu wanahabari,
Moja kati ya kazi muhimu za TFDA ni kufanya uchunguzi wa kimaabara wa sampuli za bidhaa zinazodhibitiwa ili kurahisisha/kuwezesha kufanya maamuzi mbalimbali. Kupitia uchunguzi wa kimaabara, TFDA hutegemea matokeo ya ukweli wa kisayansi  (Scientific based evidence) katika kuamua kusajili bidhaa, kuingiza au kutoa bidhaa nje ya nchi na pia katika kuamua kuendelea kushikilia/kudumisha usajili wa bidhaa husika na kuziruhusu kuendelea kuwepo katika soko.
Aidha, kupitia uchunguzi wa kimaabara, TFDA huweza kubaini uwepo wa bidhaa bandia na duni na hivyo kuchukua hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa kwa umma. Kwa minajili hii Maabara ya TFDA ni chombo muhimu katika kuisaidia Menejimenti kufanya maamuzi na hivyo kutimiza wajibu wa kusimamia usalama, ubora na ufanisi wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na Vifaa tiba nchini.
Ndugu wanahabari,
Leo tumekutana hapa kwa lengo la kupeana taarifa kuhusu mafanikio  ya Maabara ya TFDA katika kulinda afya ya wananchi. Mafanikio hayo ni kama ifuatavyo;
i.             Kutambuliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO)
Maabara ya dawa ya TFDA ilifanyiwa ukaguzi na Shirika la Afya Duniani (WHO) mwezi Mei 2005 na baadaye Septemba 2010 na kufanikiwa kukidhi vigezo, hivyo kutambuliwa rasmi na WHO tarehe 18 Januari 2011.
Maana yake ni kuwa Matokeo ya uchunguzi kupitia maabara hii yanatambuliwa kimataifa.


ii.           Kupata ITHIBATI kwa kiwango cha ISO/IEC 17025:2005
Maabara ya Chakula na Mikrobiologia ilifanikiwa kupata ITHIBATI kwa kiwango cha ISO/IEC 17025:2005 kutoka taasisi ya Southern African Development Community Accreditation Services (SADCAS), iliyotolewa  tarehe 21 Septemba  2012.
Hii pia ina maana kwamba, matokeo ya uchunguzi katika maabara hii yanatambuliwa na kukubalika kimataifa.
Cheti tulichopewa ni cha miaka mitano mpaka mwaka 2017, lakini kila mwaka wakaguzi toka SADCAS watakuwa wakikagua ili kujiridhisha kwamba TFDA bado inakidhi kiwango cha ISO/IEC 17025:2005.

Ndugu wanahabari,
Ni vema kufahamu kuwa Maabara  hii ya TFDA ni miongoni mwa  maabara nne (4) za Afrika  ambazo zimepata ithibati  kutoka SADCAS katika  uchunguzi wa kimaabara kati ya 12, ambapo nane (8) zikiwa ni Maabara  zisizo za udhibiti.

Vilevile ieleweke kwamba zipo Maabara chache nyingine hapa nchini zinazofuata mfumo   huu ingawa si maabara za udhibiti.

Baada ya kufikiwa kwa mafanikio haya, Maabara hii ya TFDA ilizinduliwa rasmi na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mnamo tarehe 18 Machi 2013. 


Ndugu wanahabari,
Faida zitokanazo na  maabara ya TFDA kutambuliwa kimataifa ni pamoja na;
(i)           Wananchi kupata uhakika wa bidhaa  za chakula, dawa vipodozi na Vifaa tiba zilizo kwenye soko
(ii)          Wazalishaji kupata maabara ya kuchunguza bidhaa  zao katika maabara inayotambulika ‘’competent labs’’ ili kupunguza  hasara ya  kuzalisha bidhaa mbovu  na kisha kuiharibu
(iii)        Kutokurudia matokeo ya uchunguzi  kama maabara iliyo chunguza  imepata Ithibati  hii hupunguza gharama kubwa na muda wa uchunguzi ‘’avoid  expensive re-testing’’
(iv)         Kwa wazalishaji na wasambazaji  kupata nafasi ya kuchunguza bidhaa zao katika maabara zinazotambulika ‘’competent labs’’ na hivyo kutopoteza hadhi kwa bidhaa wanazo zalisha/ kusambaza
Kutokana na kutaambuliwa na shirika la Afya Duniani kwa maabara ya dawa na kupata ithibati kwa maabara za chakula na mikrobiolojia, Mamlaka imeanza kupata wateja kutoka nchi za nje na mashirika ya kimataifa. Nchi hizo ni pamoja na Kenya, Zambia, Rwanda, Uganda, Ethiopia, Nigeria, Cameroon, Ghana na Botswana. Kwa kulitambua hili, TFDA iko katika hatua za mwisho za kuandaa mpango maalumu wa kuboresha huduma za maabara (business plan) ili kukidhi mahitaji ya wateja wa ndani na nje.  Mpango huu umepitia upya muundo wa maabara, taratibu za utoaji huduma, mahitaji ya vifaa na wataalamu.  Lengo kuu ni kuongeza tija bila kuathiri dhima ya TFDA ya kulinda afya ya jamii.

Ndugu wanahabari,
Tangu kuanzishwa kwa maabara ya TFDA mwaka 2003 hadi Machi 2013, Sampuli mbalimbali zimeweza kuchunguzwa katika maabara ya TFDA kama ifuatavyo; chakula (5,173), dawa (6,163), vipodozi (307) na Vifaa tiba (36).
Kupitia mfumo wa Ufuatiliaji wa dawa (PMS) kwa lengo la kujiridhisha na usalama, ubora na ufanisi wa dawa, katika kipindi cha Julai 2008 - Desemba 2012, jumla ya sampuli 1,827 zilichukuliwa katika soko na kuchunguzwa katika maabara ya TFDA ambapo sampuli 1,670 (97%) zilikidhi vigezo.

Aidha, kupitia Matokeo ya uchunguzi wa kimaabara katika kipindi cha takriban miaka 10 sasa (2003 – 2013) bidhaa mbalimbali duni na bandia ziliweza kubainika na kutolewa katika soko kama ifuatavyo; bidhaa za chakula (84), bidhaa za dawa (71), bidhaa za vipodozi 2,764 na  bidhaa za vifaa tiba (1).

Naamini uzoefu wa miaka takribani 10 tulio nao katika uchunguzi  wa kimaabara  na upatikanaji wa ITHIBATI kutaendelea kuifanya TFDA kufanya kazi kwa ufanisi zaidi katika kutekeleza  mfumo huo wa utendaji kazi wa kimaabara ili bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba zitakazouzwa kwenye soko la Tanzania ziwe na viwango vinavyokubalika vya usalama, ubora na ufanisi.

Ndugu wanahabari,
TFDA inatoa shukurani kwa ushirikiano ambao mmekuwa mkiuonesha katika kutoa taarifa za kiudhibiti pale inapotokea pamoja na kuelimisha jamii.

Rai yangu kwenu ni kuendelea kutumia kalamu zenu katika kuwaondolea hofu wananchi kuhusu usalama na ubora wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na Vifaa tiba vilivyopo katika soko kutokana na mifumo thabiti iliyowekwa na TFDA.

Aidha, wito kwa wananchi ni kwamba ikiwa mtu atabaini au kuwa na shaka juu ya bidhaa hizo basi asisite kuwasiliana nasi kupitia ofisi zetu za Makao Makuu na za Kanda zilizipo Extenal Mabibo, Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma na Ofisi za Waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya au kutoa taarifa katika kituo chochote cha polisi kilicho jirani naye.
Asanteni kwa kunisikiliza!

No comments:

Post a Comment