TANGAZO


Thursday, March 15, 2018

JENGO LA ABIRIA KIWANJA CHA NDEGE CHA DODOMA KUBORESHWA

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia), akioneshwa na Meneja Mradi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Mhandisi Focus Kadege, jengo la abiria la Kiwanja cha Ndege cha Dodoma ambalo litafanyiwa uboreshwaji ili kuweza kuchukua abiria 100 kwa mara moja, Mkoani humo. 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhandisi Joseph Nyamuhanga (kushoto), akiteta jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Richard Mayongela wakati wa hafla ya utiaji saini wa mkataba wa kuboresha jengo la abiria katika kiwanja cha Ndege cha Dodoma. 
Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira ambaye pia ni Mbunge wa Dodoma Mjini, Mhe. Antony Mavunde, akitoa hotuba katika hafla ya utiaji saini wa uboreshaji wa jengo la abiria katika Kiwanja cha Ndege Dodoma, Mkoani humo. 
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Richard Mayongela (kushoto waliokaa) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Felix Maagi (kulia waliokaa), wakisaini mkataba wa uboreshaji wa jengo la abiria uliopo katika Kiwanja cha Ndege cha Dodoma, huku wakishuhudiwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhandisi Atashasta Nditiye (wa tatu kulia), Katibu Mkuu wa Sekta ya Ujenzi, Mhandisi Joseph Nyamuhanga (wa tatu kushoto) na viongozi wengine wa Serikali. 
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Richard Mayongela (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Felix Maagi (kulia), wakikabidhiana mkataba wa makubaliano ya uboreshaji wa jengo la abiria uliopo katika Kiwanja cha Ndege cha Dodoma mara baada ya kusaini, Mkoani humo. 

NAIBU Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, ametoa miezi miwili kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), kuhakikisha linakamilisha uboreshaji wa jengo la abiria lililopo katika kiwanja cha ndege cha Dodoma ili kuwezesha jengo hilo kuhudumia abiria wengi zaidi kwa wakati mmoja.

Ametoa agizo hilo, mkoani Dodoma katika hafla ya utiaji saini mkataba wa uboreshaji wa jengo baina na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA) na NHC na kusema  kuwa kukamilika kwake kutawezesha abiria zaidi ya 100 kuhudumiwa kwa wakati mmoja ambapo kwa sasa jengo linahudumia abiria 35.

“Mkataba tunaoshuhudia ukisainiwa leo unaitaka NHC kukamilisha mradi huu ndani ya miezi mitatu lakini niagize mradi huu ukamilike ndani ya miezi miwili kwa sababu fedha zipo na cheti mlichonacho cha daraja la kwanza kinaonyesha namna mnavyoweza kufanya kazi hii kwa haraka’ alisema Mhandisi Nditiye.

Aidha Naibu Waziri Mhandisi Nditiye ameitaka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), pamoja na maboresho hayo kuhakikisha inafanya maboresho kwa kujenga maduka ya kubadilishia fedha na bidhaa ili abiria watakaotumia kiwanja hicho hiyo waweze kupata huduma mbalimbali wakati wanaposubiria kupanda ndege.

Ameongeza kuwa Mkoa wa Dodoma kwa sasa ndio Makao Makuu ya Serikali hivyo miradi yote inayotekelezwa chini ya Wizara lazima izingatie viwango na thamani ya fedha ili kuendana na hadhi ya mji.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira ambaye pia ni Mbunge wa Dodoma Mjini, Mheshimiwa Antony Mavunde ameipongeza Serikali kwa kutekeleza mradi huo na kumuomba Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, kuwafikiria wananchi waliopisha upanuzi wa kiwanja hicho kwa kuwalipa fidia mapema.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhandisi Joseph Nyamuhanga amesema Serikali inaendelea na mipango ya kuboresha viwanja vya ndege mbalimbali hapa nchini ili kurahisisha huduma za usafiri wa anga.

Ameongeza kuwa Serikali imepanga kujenga Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa katika eneo Msalato ambapo kwa sasa wataaalam wanapitia usanifu wa kiwanja hicho na wakati wowote zabuni itatangazwa ambapo kiwanja hicho kitaweza kuhudumia ndege kubwa za kisasa kwani kinatarajiwa kuwa barabara ya kuruka na kutua ndege yenye urefu wa Kilomita 4.5 mpaka 5.

Awali akitoa taarifa yake kabla ya utiaji saini Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Richard Mayongela, amesema kuwa Fedha zinazotumika kukarabati jengo hilo ni fedha za ndani za mamlaka hivyo jengo hilo litakamilika kwa wakati na viwango.

Uboreshaji wa jengo la abiria lililopo katika Kiwanja cha Ndege cha Dodoma utagharimu takribani kiasi cha shilingi milioni 600 na utahusisha mifumo ya kisasa ya Tehama, mifumo na maji taka , mifumo ya matangazi ya ratiba za ndege pamoja na mgahawa.

Imetolewa na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

No comments:

Post a Comment