Na Mwandishi wetu
14/12/2017
TAASISI isiyo ya Kiserikali inayojihusisha na masuala ya kifedha ya Tanzania Mortage Refinance Company (TMRC) imekabidhi msaada wa shilingi milioni nane kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kuwezesha matibabu ya moyo kwa watoto wanne.
Watoto hao watafanyiwa upasuaji wa moyo wa kuziba matundu na wengine kutibiwa mishipa ya damu ambayo haipitishi damu vizuri katika moyo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Mkurugenzi wa TMRC Oscar Mgaya alisema wameguswa kuchangia fedha hizo ili kuokoa maisha ya watoto hao wenye matatzo ya moyo ambao ni Taifa la kesho.
“Tumetoa shilingi millioni nane kwa ajili ya upasuaji wa kutibu magonjwa ya moyo kwa watoto wanne, tumeguswa kutoa fedha hizi ikizingatiwa watoto wengi ni wadogo hawajafikisha hata miaka mitano na watalaam wanaeleza ikiwa hawatapatiwa matibabu hasa ya upasuaji kwa wakati muafaka wataweza kupoteza maisha”,.
“Moyo ni kiungo cha muhimu sana katika mwili wa binadamu, unaweza kukosa mguu au mkono ukaishi lakini siyo moyo, binadamu akikosa moyo hawezi kuishi”, alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Prof. Mohamed Janabi aliishukuru Taasisi ya TMRC kwa kutoa fedha hizo ambazo zitaokoa maisha ya watoto wanne wanaosumbuliwa na matatizo ya moyo.
Prof. Janabi alitoa rai kwa Taasisi zingine kuiga mfano na kuendelea kujitokeza kufadhili matibabu ya watoto ambao bado wanasubiri kufanyiwa upasuaji wa moyo.
No comments:
Post a Comment