TANGAZO


Thursday, December 14, 2017

LAPF YAN'GARA UANDAAJI WA HESABU KWA MIAKA 7 MFULULIZO

Mkurugenzi wa Fedha wa Mfuko wa Pensheni wa LAPF Bw. John Kida akizungumza na waandishi kuhusu mfuko huo kupata tuzo ya uandaaji bora wa hesabu katika sekta ya hifadhi ya Jamii na Bima ya Afya kwa mwaka 2015/2016 ambapo Mfuko huo umeshika nafasi ya kwanza,  Tuzo hiyo imetolewa na  Bodi ya Taifa ya Uhasibu (NBAA) hivi karibuni.Kulia ni Meneja Masoko na Uhusiano wa LAPF Bw. James  Mlowe. (Picha zote na LAPF)
Meneja Matekelezo wa Mfuko wa Pensheni wa LAPF  Bw. Victor Kikoti (wa kwanza) akieleza kwa waandishi wa habari (hawapo pichani ) kuhusu mafao yanayotolewa na mfuko huo na faida wanazopata wananchi kutokana na mafao hayo. 

Na Mwandishi Wetu
MFUKO wa Pensheni wa LAPF umepata tuzo ya uandaaji bora wa hesabu katika sekta ya Hifadhi ya Jamii na Bima kwa mwaka 2015/16 inayotolewa na Bodi ya Taifa ya Uhasibu (NBAA).

Akizungumza  na waandishi wa habari leo Mjini Dodoma kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo Bw. Eliud Sanga,  Mkurugenzi wa fedha wa Mfuko huo Bw. John Kida amesema kuwa mfuko huo umepata tuzo hiyo kwa miaka saba mfululizo ikiwa ni ishara ya utendaji mzuri na wenye kuchochea ukuaji wa Mfuko  na maendeleo ya Taifa kwa ujumla kutokana na uwekezaji unaofanywa katika sekta mbalimbali.

“Kwa mwaka 2015/2016 mapato yanayotokana na uwekezaji katika vitega uchumi yalifikia shilingi bilioni 96.03 ikilinganishwa na shilingi bilioni 72.72 kwa mwaka 2014/2015  ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 32.” Alisisitiza Kida.

Akifafanua Kida amesema kuwa mafanikio ya mfuko huo yanatokana na kuongezeka kwa wanachama ambao hadi Septemba 2017 walikuwa wamefikia 180,401.

Aliongeza kuwa Mfuko huo katika kipindi cha mwaka 2015/2016 umelipa mafao kwa wanachama 8,011 ambapo jumla ya shilingi bilioni 107.24 zililipwa kama mafao kwa wanachama.

Akieleza mafanikio mengine Kida amesema kuwa michango ya wanachama imeongezeka ambapo kwa mwaka 2015/2016 imefikia shilingi bilioni 279.68 ikilinganishwa na shilingi bilioni 210.07 sawa na ongezeko la asilimia 33 hali iliyosababishwa na kuoongezeka kwa wanachama kutoka 150,835 hadi kufikia wanachama 166,260 mwezi June 2016.

Kwa upande wake Meneja Masoko na Uhusiano wa Mfuko huo Bw. James Mlowe amesema mafanikio ya mfuko huo yanatokana na utendaji makini unaozingatia utawala Bora katika kusimamia rasilimali za Mfuko huo ikiwemo fedha.

Mfuko wa Pensheni wa LAPF umewekeza katika vitega uchumi mbalimbali ambapo hadi kufikia June 2016 ulikuwa umewekeza jumla ya shilingi trilioni 1.09, wakati kwa kipindi cha mwezi June 2015 mfuko huo uliwekeza bilioni 884.26 katika vitega uchumi mbalimbali kama dhamana za Serikali, Amana za mabenki, majengo, hisa za makampuni  na uwekezaji katika Kampuni tanzu.

No comments:

Post a Comment