Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan
Na Paschal
Dotto-Maelezo
SERIKALI ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania imejipanga kushirikiana katika nyanja za Kiuchumi,
Utamaduni na Ulinzi na Serikali ya Oman ili kuwezesha maendeleo ya biashara
baina ya nchi hizi mbili pamoja na Pwani ya nchi za Afrika Mashariki.
Akizungumuza Jijini
Dar es Salaam leo wakati alipokutana na ujumbe wa Mfalme wa Oman Sheikh Sultan
Qabous Bin Said, Makamu wa Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema
kuwa ugeni huo ni wa aina yake kwani utaimarisha masuala ya biashara kwa nchi za
ukanda wa Pwani ya Afrika Mashariki.
Katika mazungumzo
hayo ambayo yalifanyika katika meli maalum ya Oman iitwayo Fulk Al Salamah na
kuambatana na chakula cha mchana, ujumbe wa Oman uliongozwa na Waziri wa Mafuta
na Gesi wa nchi hiyo Dkt. Mohammed Hamed Al- Rumhi.
“Huu ni ujumbe
maalumu kutoka kwa Mfalme wa Oman ambaye ametuma salamu maalum za ushirikiano
kwa wananchi wa Tanzania na nchi za Afrika Mashariki na sisi tunaupokea ugeni
huu na kujipanga kushirikiana na Serikali ya Oman katika nyanja za kiuchumi,
kiutamaduni na ulinzi na usalama kwa nchi za Pwani ya Afrika Mashariki” alisema
Mhe. Suluhu.
Aidha ameishukuru Serikali
ya Oman kwa kuonesha utayari wake wa kufanya kazi na nchi ya Tanzania pamoja na
ukanda wa Pwani ya Afrika Mashiriki na kuuhakikishia ujumbe huo kuwa Tanzania
na nchi za Pwani ya Afrika Mashariki zitaendelea kushirikiana Oman.
Makamu wa Rais
alibanisha kuwa Tanzania na Oman ni marafiki wa muda mrefu na nchi mbili hizo
zimesaini mikataba mbalimbali ya ushirikiano ambapo aliahidi kuendelea
kuifanyia kazi.
“Siyo mara ya kwanza kwa serikali ya Oman kuja
Tanzania kuna mikataba kadhaa ambayo inaimarisha uhusiano hususani kwenye
biashara na uwekezaji kwa hiyo ugeni huu ni muhimu kwa nchi yetu” Alisisitiza
Mhe. Suluhu.
Kwa upande wake, Waziri
wa Maliasili ya Utali Dkt. Hamis Kigwangala alisema kuwa ugeni huo kwa Wizara hiyo utatoa fursa ya
kujifunza kwa kuangalia Serikali ya Oman
inafanya nini ili kuweza kuimarisha Sekta ya Utalii nchini.
“Tumekuja kuangalia
na kujifunza wenzetu wanafanyaje katika mbinu za sekta ya utalii kwa mfano
serikali ya Oman ina tembelewa na watalii zaidi ya milioni 3.2 kwa mwaka lakini
kwa Tanzania sisi tunatembelewa na watalii milioni 1.2, kwa hiyo ugeni huu
utaimarisha ushirikiano wa pamoja na Oman katika sekta hii”, alisema Dkt. Kigwangala.
Aidha Dkt. Kigwangala
alisema wataanzisha ushirikiano wa mradi wa watalii kuja moja kwa moja kutoka
Oman mpaka Tanzania na Pwani ya nchi za Afrika Mashariki.
Naye Waziri wa Nishati
Dkt. Medard Kalemani alisema kuwa ujio wa ugeni huo kutoka Oman ni fursa nzuri
ya kufanya utafiti wa maeneo ya mafuta kwani serikali ya Oman ni wazoefu na wajuzi
katika masuala ya uchimbaji mafuta.
“Tunatarajia ujio huu
utajenga uhusiano mzuri katika hatua za utafiti wa mafuta hapa nchini ili
kuweza kujenga uzoefu kwa watafiti wetu na kuwawezesha watanzania kuchimba
mafuta bila shida kwa sababu wenzetu ni wazoefu katika eneo hili la kiuchumi”,
alisema Dkt. Kalemani.
Aidha Dkt. Kalemani
alisema kuwa serikali ya Oman wao watajifunza masuala ya gesi asilia kutoka Tanzania
kwa hiyo ugeni huo mkubwa ni muhimu kwa nchi zote mbili.
No comments:
Post a Comment