Na Judith Mhina- Habari Maelezo
IDADI ya watalii katika
Hifadhi ya Taifa ya Visiwa vya Rubondo imeongezeka kutoka watalii 452 kwa kipindi cha miaka 10 na kufikia 879 ndani ya mwaka mmoja, kutoka Julai 2015 mpaka Juni 2016.
Katika mahojiano maalum
na Idara ya Habari MAELEZO, Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi hiyo Bw Ignace Gara alieleza kuwa kati ya watalii 879
waliotembelea hifadhi hiyo 525 ni kutoka nje ya nchi na 354 ni wa ndani. Aidha, kwa mwaka 2005
Julai mpaka Juni 2015 watalii 452 waliotembelea
hifadhi hiyo wageni kutoka nje walikuwa ni 380
na wa ndani 72.
Bw Gara alifafanua kuwa
sababu kubwa ya ongezeko la watalii ni pamoja na hatua ya uongozi kuitangaza
hifadhi hiyo hasa kupitia mitandao ya
kijamii na uwepo wa migodi mingi katika kanda ya ziwa kama vile Migodi ya
dhahabu ya Geita, Kahama na Buzwagi ambapo baadhi wa watumishi wa migodi hiyo
wakiwemo wageni hutumia muda wa mapumziko kutembelea hifadhi hiyo.
Aidha, alitaja zoezi
la wataalamu wa wanyama pori kutoka
Ulaya la kuwafundisha Sokwe mtu waliopo hifadhini kuzoea binadamu kuwa ni miongoni mwa sababu za ongezeko hilo la
watalii katika hifadhi hiyo.
Nzohe jike, mnyama ambaye anapatikana katika hifadhi ya visiwa vya Rubondo pekee nchini.
Bw. Gara amesema: “Rubondo
ni nyumbani kwa aina pekee ya mnyama Nzohe hapa Tanzania wenye asili ya Afrika
ya Kusini, ndege aina 400, samaki aina 13, Sokwe mtu wa asili ya Afrika ya Magharibi na misitu
minene mikubwa ya asili ya Kongo.
“Hifadhi ina utajiri
mkubwa wa aina mbalimbali za ndege na samaki kama Sato, Sangara, Ngege, Mbiru,
Furu, Ningu, Kuyu, Mbofu au Hongwe, Domodomo au Mbete, Soga, Gogogo,
Kambale mumi, Kambale mamba au Kamongo, na Dagaa”. Baadhi ya aina samaki
alieleza bw. Gara kuwa wanakuwa wakubwa hadi kufikia hadi kilo 100.
Hifadhi ya Rubindo
inasifika kwa kuwa ni makaazi ya aina nyingi za ndege wakiwemo Zumbuli,
Chechelee na Taisamaki. Pia ni makazi ya aina nyingi ya ndege wa majini na
fukwe zilizojaa rasilimali za uoto wa asili wenye harufu nzuri ya kipekee.
Aidha uwepo wa mnyama
pekee katika hifadhi za Tanzania Nzohe
na Pongo ambao huvinjari katika fukwe mwanana za visiwa vya Rubondo, ‘fish
maji’ na upande wa eneo la kulala watalii Tourist Bandaz, ni kati ya vivutio vikubwa
vinavyofanya watalii wengi wa nje na ndani kutembelea hifadhi hii.
Aliongeza kwa kusema :
“Kichocheo kikubwa kwa ustawi wa wanyama na ndege katika hifadhi hii ni
upatikanaji wa malisho, maji, matunda asilia, vipepeo, wadudu na mbegu za
nafaka asilia kwa mwaka mzima. Kwa hivyo ukiwa ndani ya kisiwa utaona mandhari
nzuri ya ziwa Victoria”.
Nzohe dume, mnyama ambaye anapatikana katika hifadhi ya visiwa vya Rubondo pekee nchini.
Akielezea historia ya Hifadhi
ya Taifa ya visiwa vya Rubondo Bw Gara amesema “Historia ya hifadhi imetokana
na umuhimu wa kuhifadhi wanyama katika kisiwa hicho ambacho wakaazi wake
walijulikana kama Banyarubondo ambao walilazimika kuondolewa 1964 ili kupisha
hifadhi kufuatia tangazo la waziri mwenye dhamana ya masuala ya maliasili”
Kwa mujibu wa Bw Gara kazi
ya kuwaondoa wananchi hao ilikamilika mwaka 1965 baada ya wananchi hao kulipwa
fidia na mwaka uliofuata (1966) Rubondo ilitangazwa kama pori la akiba na miaka
10 baadaye, yaani mwaka 1977 ikapandishwa daraja na kuwa hifadhi ya
taifa.
Ni vyema kueleza hapa pia kuwa uamuzi
huu wa serikali wa kuanzisha hifadhi hiyo ulichangiwa pia na matokeo ya utafiti
uliofanywa na Shirika la Frankfurt Zoological Society la Ujerumani uliobaini hatari
ya baadhi ya wanyama kutoweka duniani wakiwemo wanaopatikana katika kisiwa
hicho.
Muikolojia wa hifadhi Bw Wickson Kibasa amesema
miaka ya 1960, dunia ilianza kupata wasiwasi kuwa baadhi ya wanyama wangeweza
kutoweka dunia. Hivyo, wataalam wa Ikolojia waliangalia uwezekano wa kuhamisha
baadhi ya wanyama kama sokwe mtu, tembo na wengine kuwapeleka nchi za Ulaya
ikiwamo Ujerumani, lakini baada ya kufananisha/kulinganisha uhalisia wa
mazingira na uoto wa asili wa Afrika Mashariki wakapendekeza sehemu pekee
duniani ya kuhifadhi wanyama hao na wanapoweza kuishi sawa na maeneo yao ya
asili ni Rubondo.
Bw Kibasa alifafanua kwa kusema, wakati
katika maeneo mbalimbali ya hifadhi barani Afrika ikiwemo Tanzania, baadhi ya wanyama kama tembo
wanapotea kwa ujangili, hali ni tofauti katika Hifadhi ya Rubondo. Kila mwaka
tembo waliopandikizwa wanaongezeka na wanyama kama, twiga, sokwe mtu, nzohe,
ngedere weusi, weupe, mamba na viboko na
wanyama wengine walipandikizwa Rubondo wanaongezeka.
Mkuu wa Hifadhi Bw
Gara, alihitimisha kwa kusema: “Ili kuondoa
changamoto za uvamizi, ujangili na uharibifu wa mazingira Hifadhi imejikita katika kutekeleza maagizo
ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa namnukuu:
“Kutoa elimu ya
uhamasishaji wa jamiii kulinda na kuheshimu mipaka yote ya vijiji vyote
vinavyozunguka hifadhi nchini kwa lengo la kuondokana na migogoro mingi
iliyokuwa ikijitokeza baina vijiji vya jirani na hifadhi”.
Waziri Mkuu alitoa
maagizo haya, alipokuwa kwenye ziara yake Mkoani Manyara hivi karibuni na
hifadhi yetu inatekeleza kikamilifu. Pia alisisitiza utakelezaji wa ilani ya Chama
cha Mapinduzi ya kuongeza na kuboresha mazali ya samaki katika maeneo owevu au
chepechepe ili kuwaletea wananchi uhakika wa chakula na kipato.
Katika kutekeleza agizo
la Waziri Mkuu, Kitengo cha Ujirani mwema cha Rubondo “Kinatoa elimu ya uhifadhi katika jamii zinazopakana na
hifadhi, kupitia elimu hiyo wananchi wamekuwa wakielimishwa kuhusu madhara ya
uvuvi haramu katika ziwa Victoria na mbinu za uvuvi endelevu ndani ya ziwa”. amesema
Bw David Kadomo, ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Ujirani mwema.
Aidha, “Hifadhi kwa
kushirikiana na maafisa uvuvi katika wilaya zinazopakana na hifadhi yetu,
tumekuwa tukiwaelimisha wananchi na kuhimiza utunzaji wa ardhi oevu kwenye
mialo za ziwa Victoria”.
Akifafanua mkakati huo Bw
Kadomo amesema hifadhi: ‘Imeandaa mpango kwa kushirikiana na wananchi katika
mialo ya Bulongero kata ya Izumacheli wilaya ya Geita, Kabiga kata ya Maisome
wilaya ya Sengerema, Kasenyi kata ya Ikuza wilaya ya Muleba na Mwerani kata ya Mganza wilaya ya Chato katika
kuboresha na kuongeza vituo vya mazalia ya samaki katika mialo hiyo.
Matarajio ya Hifadhi ni
kuboreshwa kwa mazalia ya samaki na kuanzisha vituo mbalimbali kando kando mwa
ziwa ili, wananchi kuzalisha samaki kwa wingi kama azma ya serikali ilivyokusudia
na kuondoa changamoto ya kutoweka kwa samaki wenye uzito mkubwa unaotakiwa
viwandani, hii itapunguza kama si
kuondoa kabisa, kasi ya watu kuja
kufanya uvuvi kwenye maeneo ya Hifadhi.
Bw Kadomo alimalizia na
kusema: “Kitengo cha Ujirani Mwema kinaandaa ziara za makundi mbalimbali ya
jamii kuja kutembelea hifadhi na kuona vivutio mbalimbali ndani ya hifadhi.
Makundi haya yamekuwa yakihusisha wanafunzi wa shule za msingi na sekondari
zinazo jirani na hifadhi”.
Aliendelea kwa kusema:“Makundi
mengine ni viongozi wa serikali za vijiji na kata zinazopakana na hifadhi”.
Hifadhi ya Rubondo, kijografia ipo Mkoa wa Geita, imezungukwa na visiwa 11 vidogo vidogo ambapo
ni sehemu ya hifadhi, kuna majabali
makubwa 2; moja upande wa kaskazini
na lingine upande wa kusini ndani ya misitu minene ya asili ya Kongo.
Hifadhi ya Taifa ya visiwa vya Rubondo ipo
jirani na visiwa kadhaa vya makazi ambayo ni Mizo, Nyamitundu, Chitende,
Katera, Iroba, Chambuzi, Munyila, Makosi, pamoja na Izilambula. Rubondo ni
hifadhi pekee nchini Tanzania na Barani Afrika ipatikanayo katika makazi ya
maji ya Ziwa. Kijografia hifadhi hii inapatikana katika Ziwa Victoria Kaskazini
mwa ghuba ya Emini pasha Mkoani Geita.
Hifadhi ya Rubondo ina
ukubwa wa kilometa za mraba 457, ambapo kilometa za mraba 237 ni nchi kavu na
220 kilometa za mraba ni maji. Hifadhi hii ipo ndani ya ziwa Victoria ambalo ni
la pili kwa ukubwa duniani, lenye
kilometa za mraba 69,485, likitanguliwa na ziwa Superior la Amerika ya
Kaskazini lenye ukubwa wa kilometa za
mraba 82,414.
Mwisho Watanzania
wasikubali kusoma au kuhadithiwa juu ya
Hifadhi ya Taifa ya Visiwa vya Rubondo nenda na ujionee kwa macho. Tuthamini na
kuzitunza Hifadhi zetu, kwa vizazi vya sasa na vya baadaye. Hifadhi inafikika
kwa njia ya usafiri wa maji ya Ziwa Victoria ni takriban kilometa 165
kutoka Sengerema kuelekea hifadhi, na
kutoka Geita na Nzera kuna umbali wa kilometa 6 mpaka 7.
No comments:
Post a Comment