Mgeni Rasmi Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa katika picha
ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam wakati wa
sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Miaka 55 tangu Chuo hicho kianzishwe,
sherehe hizo zimefanyika katika ukumbi wa Nkrumah, Kampasi ya Mwalimu J. K.
Nyerere (Mlimani) mapema hii leo.(Picha zote na Eliphace Marwa - Maelezo)
Na Frank Shija,
MAELEZO.
UDSM washauriwa
kutumia maadhimisho ya miaka 55 tangu kuanzishwa kwa Chuo hicho kufanya
tathmini ya mafanikio na changamoto walizokumbana nazo katika kipindi
kilichopita ili kujiwekea malengo ya maendeleo ifikapo 2061.
Rai hiyo imetolewa na
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (MB)
katika hafla ya kufunga maadhimisho ya
miaka 55 ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) yaliyofanyika katika
ukumbi wa Nkurumah leo Jijini Dar es Salaam.
“Leo ni siku ambayo
tunahitimisha Maadhimisho ya miaka 55 tangu kuanzishwa kwa Chuo hiki, ni vyema
basi tukatumia sherehe hizi kufanya tathmini ya mafanikio na changamoto
mlizokumbana nazo kwa kipindi kilichopita”. Alisema Mhe. Majaliwa.
Awali akisoma hotuba
yake Waziri Mkuu Majaliwa alitumia fursa hiyo kuelezea namna ambavyo Serikali
ya Awamu ya Tano ilivyojipanga kuhakikisha inafanya maboresho makubwa katika
taasisi za elimu za umma ikiwamo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Alizitaja baadhi ya
changamoto na namna ambavyo Serikali imekuwa ikizishughulikia kuwa ni pamoja
na; Maslahi ya watumishi, wanataalamu na waendeshaji ambapo alisema Serikali
inatambua uwepo wa madai mbalimbali ikiwa ni pamoja na malimbikizo ya mishahara,
na kuongeza kuwa suala hilo tayari limekwisha anza kushughulikiwa kwa kuchukua
hatua kadhaa ikiwemo zoezi la uhakiki wa wafanyakazi na watumishi hewa.
Kuhusu changamoto ya
uhaba wa Wahadhiri Waandamizi na Maprofesa katika Vyuo vya Umma, Majaliwa
alisema Serikali itaendelea kuweka kipaumbele cha upatikanaji wa fedha za
kutosha kwa ajili ya mafunzo na kuvitaka Vyuo navyo viweke taratibu na mipango
endelevu ya kurithishana ili kupunguza ombwe lililopo.
Akizungumzia kuhusu
mikopo ya Elimu ya Juu, Waziri Mkuu amesema kuwa tayari Serikali kupitia Mhe.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli imetoa
ufafanuzi wa namna utekelezaji wa kutoa mikopo hiyo, na Wizara yenye dhamana
inaendelea na uhakiki wa taarifa za waombaji wa mikopo. Alitoa wito kwa
wanufaika na waombaji wote wa mikopo wahakikishe wanawasilisha taarifa sahihi
na za uhakika.
Nakuongeza kuwa
Serikali imekwisha ongeza bajeti ya mikopo ya Elimu ya Juu kutoka shilingi
bilioni 340 mwaka 2015/2016 hadi bilioni 483 kwa mwaka 2016/2017 hivyo hakuna
mwanafunzi anyestahili kupata mkopo atakayekosa.
Awali akisoma
historia ya chuo hicho Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa
Rwekaza Mukandala alisema kuwa maadhimisho hayo wanayatumia kufanya tathmini ya
safari ya Chuo kuelekea maendeleo ya karne moja ifikapo mwaka 1961.
Profesa Rwekaza
amesema kuwa kumekuwa na mabadiliko makubwa katika ukuaji wa Chuo hicho
uliotokana na mahitaji kulingana na wakati husika na kuongeza kuwa lengo kubwa
la uongozi ni kuhakikisha Chuo hicho kinaendela kuwa kinara katika kutoa elimu
bora kulingana na wakati.
Aliongeza kuwa pamoja
na changamoto kadhaa walizokumbana nazo Chuo hicho kimekuwa daraja muhimu la
kuzalisha wanataaluma ambapo takribani wanataaluma 90,000 wa ndani na nje ya
nchi wametokana na chuo hicho.
Naye Naibu Katibu
Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo
akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo, Profesa Joyce Ndarichako
amesema kuwa Serikali itaendelea kushughulikia changamoto zinazoikabili sekta
ya elimu nchini.
Ameongeza kuwa wizara
imekuwa ikiendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuhudumia sughuli mbalimbali za
maendeleo ya elimu na kuongeza kuwa hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania aliweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa mabweni ambao
unatarajiwa kukamilima ifikapo Desemba 2016.
Mradi huo
utakapokamilika utakuwa upunguza changamoto ya uhaba wa mabweni kwa wanafunzi
na kuwaondolea hadha ya kuishi mitaa, huku mabweni hayo yakitarajiwa kutumiwa
na wanafunzi takribani 3840.
Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam kinaadhimisha miaka 55 tangu kuasisiwa kwake mnamo mwaka 1961 huku
kikianzia katika majengo ya TANU( sasa hivi CCM) yaliyoko mtaa wa Lumumba
jijini Dar es Salaam kabla ya kuhamia katika eneo la Mlimani mnamo mwaka 1964.
No comments:
Post a Comment