TANGAZO


Thursday, August 25, 2016

WATAALAMU WA TEHAMA WATAKIWA KUWA NA MAADILI

Naibu Waziri  Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akiongea na wataalamu wa Tehama wakati wa uzinduzi wa mkutano wa siku moja wa wataalamu hao, uliofanyika jijini Dar es Salaam leo. (Picha zote na Benjamin Sawe)
Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano anayeshughulikia Sekta ya Mawasiliano, Prof. Faustine Kamuzora  akiongea na wataalam wa Tehama wakati wa uzinduzi wa mkutano wa siku moja wa wataalamu hao uliofanyika jijini Dar es Salaam leo. 
Naibu Waziri  Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani  akiongea na wanahabari (hawapo pichani), wakati wa uzinduzi wa mkutano wa siku moja wa wataalamu hao uliofanyika jijini Dar es Salaam leo. 
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo, wakisikiliza maelezo mbalimbali yaliyokuwa yakitolewa.

Na Abushehe Nondo, Maelezo.
NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani ameiagiza Tume ya Teknolojia ya Habari na  Mawasiliano nchini kuhakikisha wanatengeneza misingi ya uadilifu wa kitaaluma na misingi hiyo itumike kuwadhibiti wale ambao wanatumia utaalamu huo kwa nia ovu.

Mhandisi Ngonyani aliyasema hayo, wakati akizindua mkutano wa kwanza ambao umeandaliwa ma Tume mpya ya Teknolojia, Habari na Mawasiliano (TEHAMA), uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa  Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

Alisema Mkutano huo una lengo la kuwakutanisha wataalamu wa TEHAMA kutoka katika sekta za umma na sekta binafsi ili kuweza kujadiliana ni kwa namna gani taaluma hiyo inavyoweza kutumika zaidi kwa faida ya ukuaji wa uchumi nchini Tanzania.

“Wapo baadhi ya watu wanatumia taaluma ya TEHAMA kwa manufaa mbalimbali ya kujenga uchumi na maendeleo, lakini wapo wachache ambao wanatumia utaalamu wao kwa manufaa  binafsi ikiwemo kuwadhalilisha watu wengine na kuwaibia fedha zao katika mitandao” Alisema Mhandisi Ngonyani.

Alisema Tume hiyo ya Teknolojia ya Habari na  Mawasiliano inatakiwa  kuja na sheria kali ambazo zitawabana wale wote ambao wamekua na tabia ya kutumia mitandao katika kufanya vitendo viovu badala ya kutumia katika kujiletea maendeleo.

Awali akizungumza katika mkutano huo,  Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi , Uchukuzi na Mawasiliano upande wa sekta ya Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora alisema uanzishwaji wa Tume ya Teknolojia ya Habari na  Mawasiliano nchini ni jitihada za makusudi za serikali  katika kukuza Mawasiliano.

Prof. Kamuzora alisema kuwa tume hiyo ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Taifa na hivyo kuwasihi watendaji hao kuwaelimisha zaidi wananchi  kujikita zaidi katika kufuata maadili ya taaluma hiyo ili kulifikisha Taifa katika mafanikio ya sekta  ya mawasiliano.


Alisema Tume ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano itasaidia kukuza uchumi wa Taifa kutokana na kukua kwa sekta ya TEHAMA na kuchochea uzalishaji ,ukuaji wa sekta zingine kiuchumi na usambazaji wa huduma za jamii.

No comments:

Post a Comment